islamkingdomface islamkingdomtwitte islamkingdominstagram islamkingdompinterest islamkingdomtumblr islamkingdomreddit islamkingdomvk


KUAMINI MAJINA YA MWENYEZI MUNGU SUBHANA WATAALA


19064
wasifu
Kuamini majina ya Mwenyezi Mngu na sifa Zake ni msingi mkubwa kati ya misingi ya Dini na ni sababu maja kati ya sababu za mtu kuingia Peponi . Na Mwenyezi Mngu Mwenye baraka na tukuka Amewahimiza waja wamuombe na wamlinganie kwa majina Yake mema na sifa Zake tukufu. Kwa hivyo inatakiwa kwa kila Muislamu ajifunze majina hayo na sifa hizo na aelewe maana yake.
Khutba ya

Utangulizi

Shukran ni za Mola wa viumbe vyote.Rehma na amani zimfikie Mtume Muhammad. Tutazungumzia katika khutba hii tukufu tutahimizana juu ya kuamini majina ya Mwenyezi Mungu pia tutafafanua maana ya baadhi ya majina ya Mwenyezi Mungu tutaendelea kuhimizana kuomba dua kwa majina ya Mungu vile vile tutaweka wazi ya kwamba majina ya Mwenyezi Mungu ni kulingana na Quran na hadithi za Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam).

Ama baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu na kumtakia rehma na amani Mtume Muhammad. Ni lazima kwa kila Muislamu aamini kuweko kwa Mwenyezi Mungu na kuamini kuwa Mwenyezi Mungu Ndie Aliyeumba kila kitu na yeye ndiye Anayeupeleka ulimwengu na anafanya atakalo. Pia ni wajibu kwa Muislamu kuamini kwamba Mwenyezi Mungu Ndiye anayestahiki kuabudiwa peke Yake kama ambavyo inatakiwa kwa Muislamu kuamini kwamba Mwenyezi Mungu hafanani na yoyote katika majina Yake na sifa Zake. Muislamu akiamini haya tuliyoyataja basi imani yake kwa Mwenyezi Mungu itakuwa imekamilika.

Enyi waja wa Mwenyezi Mungu munaonisikiliza, Hakika ni katika kumuamini Mwenyezi Mungu kuamini majina Yake mazuri na sifa zake tukufu bila ya kufananisha wala kuzipuuza.

)وَلِلَّهِ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَى فَادْعُوهُ بِهَا) [الأعراف: 180]

Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Mwenyezi Mungu Ana majina mazuri, muombeni kwa majina hayo}} [Al-Araaf : 180]. Katika maneno haya tunapata faida kwamba haifai kwa yoyote kubadilisha jina lolote au sifa yoyote ya Mwenyezi Mungu kwa sababu yoyote ile na pia haifai kufananisha jina au sifa ya Mwenyezi Mungu na jina au sifa ya mtu yoyote. Kwani kufanya hivyo ni kumfanya sawa Mwenyezi Mungu na kiumbe wake, Vilevile haifai kabisa kusema kwamba jina ambalo Mwenyezi Mungu Amelithibitisha au Mtume wake (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) jina hilo au sifa hiyo. Ni vyema kwa Muislamu ayajue majina ya Mwenyezi Mungu na amuombe kwa majina hayo.

Misingi Muhimu ya Majina na Sifa za Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala)

Ndugu katika imani! Nafurahi kukutajia baadhi ya misingi inayohusiana na majina hiyo;

Majina ya Mwenyezi Mungu yote ni mazuri tena yamefikia kilele katika uzuri kwa kule kukusanya kwake sifa zilizokamilika zisizo na upungufu ndani yake kwa namna yoyote.

قال تعالى : )وَلِلَّهِ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَى فَادْعُوهُ بِهَا) [الأعراف: 180].

Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Mwenyezi Mungu Ana majina mazuri, muombeni kwa majina hayo}} [Al-Araaf : 180].

Majina ya Mwenyezi Mungu ni yale aliyojiita kwa majina hayo au aliyomwita yeye Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) na haifai kwa mtu yoyote kutunga jina na kumpa Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala). Inavyotakiwa ni mtu kumwita Mwenyezi Mungu majina aliyojiita Mwenyewe katika kitabu chake na yale ambayo Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) katika hadithi zake tukufu, wala hafai mtu kuzungumza jambo bila ya ujuzi.

قال تعالى) : وَلَا تَقْفُ مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ ([الإسراء: 36] Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) Asema: {{Wala usizungumze jambo ambalo huna ujuzi nalo, hakika masikio na macho na moyo kutaulizwa kuhusiana navyo}} [Al-Isra : 36].

Majina ya Mwenyezi Mungu hayana idadi maalumu. Muislamu atakiwa alijue hili vizuri kabisa, na hii ni kwa mujibu wa hadithi ya Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) aliposema: [ Ewe Mwenyezi Mungu na kuomba kwa kila jina ambalo liko kwenye kitabu chako, au ulilomfundisha yoyote katika viumbe vyako, au ulilolificha katika elimu isiyojulikana na yoyote kwako]. Katika majina ambayo Mwenyezi Mungu hakuyataja wala hakuyafundisha viumbe nakuonesha kwamba majina yake hayana idadi maalumu.

Baada ya kutaja misingi muhimu ambayo yatakiwa kwa Muislamu aifahamu vizuri ili imani yake kwa Mwenyezi Mungu hususan katika majina yake na sifa zake iwe imekamilika vyema.

Maana ya Majina ya Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala)

Nachukua tena nafasi nyengine kufafanua baadhi ya majina ya Mwenyezi Mungu. Na katika majina hayo ni:-

(ALLAH ) ni muabudiwa wa haki kwa mapenzi yote katika ibada hiyo katika hali ya kumtukuza.

(MWINGI WA REHMA MWENYE KUREHEMU) ni Ambaye anawahurumia zaidi waja wake kuliko mzazi kumhurumia mwanawe, kwani neema yoyote inayopatikana ni kwa huruma ya Mwenyezi Mungu na hakuna dhara lolote lililomuepuka mwanadamu, pia ni kwa rehma ya Mwenyezi Mungu.

قال تعالى : (وَمَا بِكُمْ مِنْ نِعْمَةٍ فَمِنَ اللَّهِ ) [النحل: 53]

Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Na hakuna neema yoyote isipokuwa yatoka kwa Mwenyezi Mungu}} [An-Nahal : 53].

(MFALME) Mwenye kumiliki ulimwengu wote juu yake na chini kiasi kwamba hakitikisiki chochote isipokuwa Anajua bali yeye Ndiye Aliyetaka kitikisike.

قال تعالى): مَالِكِ يَوْمِ الدِّينِ) [الفاتحة: 4]

Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Mfalme siku ya malipo}} [Al-Faatiha : 3].

(MTAKATIFU) ni aliyetakasika na upungufu waliyonao viumbe vyake, kwani Mwenyezi Mungu hapatwi na uchovu wala maafa yoyote kinyume na mwanadamu hupatwa na machovu na pia maafa.

قال تعالى : (وَلَقَدْ خَلَقْنَا السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَمَا بَيْنَهُمَا فِي سِتَّةِ أَيَّامٍ وَمَا مَسَّنَا مِنْ لُغُوبٍ) [ق: 38]

.

Amesema Mola (Subhaanahu wa Taala): {{Na hakika si lingine tumeziumba mbingu na ardhi zilizo kati yake na hatukupatwa na uchovu}} [Qaaf : 38].

(MWENYE NGUVU MTENDESHA NGUVU) hakuna kiumbe chochote isipokuwa kiko chini ya uwezo Wake pia kinamyenyekea Yeye.

قال تعالى : (مَا قَدَرُوا اللَّهَ حَقَّ قَدْرِهِ إِنَّ اللَّهَ لَقَوِيٌّ عَزِيزٌ) [الحج: 74]

Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Na hawakumjua Mwenyezi Mungu haki ya kumjua hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu Asiyeshindwa na yoyote}} [ Al-Hajj : 74].

(MJUZI) ni Ambaye yuwajua siri na kilichodhihiri na anajua kilicho bara na baharini na anajua kila kitu Ametakasika Mwenyezi Mungu.

(MTUKUFU ALIYE JUU) Aliye juu kwa dhati Yake juu ya Arshi na pia ni Mtukufu kwa sifa zake.

(ANAFANYA ATAKALO) Mwenye uwezo wa hali ya juu wa kufanya lolote analolitaka.

(MWENYE KUSAMEHE) Anayesamehe makosa yote aliyotendewa na anayesitiri aibu hata zikiwa nyingi kiasi gani. Amesema Mola katika Hadithi Qudsi: [ Ewe mwanadamu, hakika yako wewe utakachoniomba na ukatarajia basi nimekusamehe dhambi zote wala sijali].

(MWENYE HEKIMA) Anayeweka vitu pahali pake na anayekadiria vitu vizuri.

(MWENYE KUJITOSHELEZA) Anayejitosheleza mwenyewe asiyehitajia yoyote katika viumbe. Majina haya ndio nimeona niwafafanulie kwa uchache lakini majina mengine mengi ya Mwenyezi Mungu nimeyaacha kulingana na wakati

Enyi waumini, mnaonisikiliza! yamekuja mahimizo makubwa juu ya kuomba dua kwa majina ya Mwenyezi Mungu.

قال تعالى: (وَلِلَّهِ الْأَسْمَاءُ الْحُسْنَى فَادْعُوهُ بِهَا) [الأعراف: 180]

Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Mwenyezi Mungu Ana majina mazuri, muombeni kwa majina hayo}} [Al-Araaf : 180]. Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) amebainisha namna gani tutamuomba Mwenyezi Mungu kupitia majina yake matukufu. Katika hadithi Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) alimsikia mtu katika maswahaba akisema: [Ewe Mwenyezi Mungu, Nakuomba wewe kwani sifa na shukrani zote ni zako, hakuna mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Wewe peke yako. Huna mshirika, Mwenye kusimulia unalofanya, Muumba wa mbingu na ardhi, Mwenye utukufu, na ukarimu, Ewe ulio hai Mwenye kusimamia kila kitu. Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) akasema: “ Hakika umemuomba Mwenyezi Mungu aliyetukuka kwa jina lake tukufu ambalo akiombwa kwa jina hilo hujibu na Akiombwa hutoa]. Kwa hivyo, ni juu yako mja wa Mwenyezi Mungu kuomba kwa majina yake.

Amesema Sheikh Muhammad Swaleh Uthaimin Allah Amrehemu katika kubainisha maana ya Neno lake Mwenyezi Mungu: “Muombeni kwa majina yake”. Amesema Sheikh: ‘Ni kuyafanya ni njia ya kupata unachotaka katika maombi, kwa hivyo, utachagua jina linalonasibiana na matakwa yako, kwa mfano ikiwa unaomba msamaha basi utasema: “Ewe Mwenye kusamehe nisamehe”. Na hainasibiani kusema: “ Ewe Mwenyezi Mungu Mkali wa kuadhibu nisamehe, bali hii ni kama kumcheza Mwenyezi Mungu shere, na inatakiwa useme «Ewe Mwenyezi Mungu Mkali wa adhabu niepushie adhabu Yako’.

Ndugu Waislamu, kinachotakiwa kwetu ni kukitegemea zaidi kitabu cha Mwenyezi Mungu na hadithi za Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) katika kuyajua majina ya Mwenyezi Mungu, kwani haifai kabisa kwa yoyote kumpa Mwenyezi Mungu jina ambalo hakujiita jina hilo wala hajamuita jina hilo Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam).

Khutba ya pili

Shukrani za dhati na sifa njema zote zinamstahiki Mwenyezi Mungu Mola wa mashariki na magharibi. Rehma na amani zimfikie Kipenzi chetu na kiongozi wetu Mtume Muhammad. Ama baada ya kumtukuza Mwenyezi Mungu na kumsifu kwa sifa zake Anazostahiki kusifiwa nazo na kumtakia rehema na amani Mtume wetu mkarimu.

Napenda kuchukua fursa nyingine katika khutba hii kuzitaja baadhi ya dua ambazo Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) alizoomba kwa majina mazuri ya Mwenyezi Mungu. Mtume asema: [ Ewe Mwenyezi Mungu wewe ni Mola wangu hakuna apasaye kuabudiwa kwa haki ila wewe umeniumba na mimi ni mja wako na niko katika dhamana yako na ahadi yako niwezavyo, narudi kwako kwa neema zako kwangu, na nirudi kwako na dhambi zangu, basi nisamehe, kwani hasamehe dhambi isipokuwa wewe. Najilinda kwako kutokamana na shari ya kila nilichofanya]. Na akasema Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam): [ Mwenye kusoma dua hii wakati wa usiku na akafa usiku huo, basi ataingia peponi].

Na Mtume alipokuwa akiswali alikuwa akisema: [Nimeuelekeza uso wangu kwa yule Aliyeumba mbingu na ardhi hali kujiepusha na shirki na hali ya kuwa mimi ni Muislamu na sikuwa katika washirikina. Hakika swala yangu na ibada zangu za kuchinja, na uhai wangu na kufa kwangu ni kwa Mwenyezi Mungu Mola wa viumbe vyote, hana mshirika na kwa hili nimeamrishwa na mimi ni Muislamu wa kwanza. Ewe Mwenyezi Mungu, Wewe ni Mfalme hakuna Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa wewe, Wewe Mola wangu na mimi ni mja wako nimejidhulumu nafsi yangu, na nimezikubali dhambi zangu zote, kwani hakika hasamehe dhambi isipokuwa wewe. Niongoze katika tabia njema, kwani hakuna mwenye kuongoza katika tabia njema ila Wewe, na uniondoshee tabia mbaya kwani hakuna mwenye kuondosha tabia mbaya ila Wewe. Nakuitikia wewe, na utukufu ni wako na kheri zote ziko mikononi mwako na shari haitegemezwi kwako. Mimi niko kwako, umetukuka na umetakasika. Nakutaka msamaha na narudi kwako].

Na Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) alikuwa akisema wakati akirukuu: [ Ewe Mwenyezi Mungu nimerukuu kwa ajili yako na nimekuamini Wewe na kwako Wewe nimjisalimisha na yamenyenyekea kwako masikio yangu, macho yangu, akili yangu, mifupa yangu na mishipa yangu]. Pia Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) alikuwa akisema anapoinuka kutoka kwenye rukuu: [ Mwenyezi Mungu Amemsikia Anayemsifu, Mola wetu, shukran ni zako wewe zilizomo mbinguni na ardhini na baina yake na katika kila kitu baada yake].

Vilevile Mtume alikuwa akisema katika sijida: [ Ewe Mwenyezi Mungu, ni mesujudu kwa ajili yako na nimekuamini wewe na nimejisalimsha kwako, umesujudu uso wangu umsujudu Aliyeumba na Akautia sura na akapasua masikio yake na macho yake. Basi Ametakasika Mwenyezi Mungu Mbora wa kuumba]. Na akimaliza kuswali anasema: [Ewe Mwenyezi Mungu, Nisamehe mimi madhambi niliyoyatanguliza na niliyoyachelewesha na niliyoyafanya kwa siri na niliyofanya kwa dhahiri na niliyoyafanya kwa wingi na unayoyajua wewe zaidi kuliko mimi. Wewe ni Mwenye kumtanguliza umtakaye, na Mwenye kumweka nyuma umtakaye, hakuna Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila wewe].

Enyi waumini wa kweli! jiepusheni na kumuita Mwenyezi Mungu majina yasiyokuwa yake bila ya ujuzi, kwani kufanya hivyo ni kuzungumza juu ya Mwenyezi Mungu bila ya elimu.

قال تعالى) : وَلَا تَقْفُ مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ). [الإسراء: 36]

Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Wala usizungumze jambo ambalo huna ujuzi nalo}} [Al-Isra : 36].

Mwisho napenda kukariri kwa kuhimiza kuyaamini majina ya Mwenyezi Mungu na kufanya vitendo ambavyo vinalingana na imani hiyo.

Enyi waumini mcheni Mwenyezi Mungu na mjue ya kwamba mnaelekea kwake, na shikamaneni na kitabu chake na mushikamane na sunna sahihi za Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam), na mumuite Mwenyezi Mungu kwa majina yake Aliyejiita, na sifa zake alizojisifu nazo, na atakaye kwenda kinyume na maamrisho yake, basi Mwenyezi Mungu Amemuahidi adhabu kali.

Mwisho

Kwa kweli tumezungumzia kuhusu kuhimizana juu ya kuamini majina ya Mungu pia tukafafanua maana za baadhi ya majina ya Mungu vile vile tukahimiza kuomba dua kwa majina ya Mungu kama ambavyo tumeweza ya kwamba majina ya Mungu ni kulingana na Quran na hadithi za Mtume rehma na amani zimfikie.

Mwisho kabisa tunamuomba Mwenyezi Mungu atujaaliye tuwe miongoni mwa wenye kusikiliza yaliomema na tuwe ni wenye kuyafuata.Tunamuomba Mwenyezi Mungu atupe imani iliyothibiti na aturuzuku matendo mazuri. Amin!





Vitambulisho: