islamkingdomface islamkingdomtwitte islamkingdominstagram islamkingdompinterest islamkingdomtumblr islamkingdomreddit islamkingdomvk


KUTAHADHARI NA UCHAWI NA UGANGA


13407
wasifu
muislamu anatakikana amuamini mwenyezi mungu na kumtegeme yeye katika mamabo yake yote,wala hafai kuamini waganga na wachawi,na yamekuja makemeo makubwa kwa wale wanao kwenda kwa waganga na kwa wachawi,na jambo hilo mtu anapo lifanya huwa amekanyusha aloletewa mtume muhamma s.a.w na na kuwa mbali na mamrisho ya mwenyezi mungu s.w
Khutba ya

Shukrani ni za Allah (Subhaanahu wa Taala), Mola wa viumbe vyote. Tunamtakia rehema na amani Mtume Muhammad. Kwa uwezo wa Mungu tutazungumzia kuhusu kufungamanisha nyoyo za Waislamu na Mola wao. Vilevile tubainishe hukumu ya uchawi na uganga katika uislamu pia tutatoa tahadhari kwa watu kwenda kwa waganga na wapiga ramli na pia tuwabainishie hatari za waganga katika umma tutahimiza kuchukua sababu za kisheria.

Ama baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala), na kumtakia rehma na amani Mtume Muhammad. Ni kweli usiofichika ya kwamba watu wanapitia mitihani mbali mbali, kwa mfano mitihani ya kiuchumi, ya kiafya na pia ya kijamii na mitihani mingineo. Kwa hivyo kukabiliana na mitihani hii ni lazima sheria ichungwe na sababu za kisheria zifuatwe katika kutatua matatizo yoyote yanayomkabili Muislamu popote alipo hafai kwenda kinyume na sheria.

Enyi waja wa Mwenyezi Mungu, hakika katika mitihani waliopewa watu leo, waume kwa wake, wakubwa kwa wadogo, isipokuwa walio rehemewa na Mwenyezi Mungu ni kwenda kwa waganga na watu wa ramli wanaokula mali za watu kwa batili. Unaweza kumuona kiongozi amefungamanishwa na mganga hafanyi jambo lolote isipokuwa kwa ushauri wake hata kama ushauri huo utaenda kinyume na dini ya kiislamu, na anahisi ndani ya moyo wake ya kwamba huyo mganga ndiye anayempa uongozi na anaweza kuuchukua uongozi huo.

قال تعالى) : قُلِ اللَّهُمَّ مَالِكَ الْمُلْكِ تُؤْتِي الْمُلْكَ مَنْ تَشَاءُ وَتَنْزِعُ الْمُلْكَ مِمَّنْ تَشَاءُ وَتُعِزُّ مَنْ تَشَاءُ وَتُذِلُّ مَنْ تَشَاءُ بِيَدِكَ الْخَيْرُ إِنَّكَ عَلَى كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ) [آل عمران: 26]

Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Sema ewe Mwenyezi Mungu Mfalme wa wafalme Unampa ufalme unaye mtaka na unampokonya ufalme unayemtaka na unamtukuza unayemtaka na Unamdhalilisha unayemtaka katika mkono wako kuna kheri. Hakika yako wewe juu ya kila kitu ni muweza}}.

Utaona mfanyabiashara hanunui wala hauzi isipokuwa kwa ushauri wa mganga ambaye amefungamanisha moyo wake na mganga huyo na hufanya lolote atakaloambiwa na mganga namna litakavyokuwa jambo lile. Utapata mke anaetaka kumtawala mumewe kwa kiasi ambacho mume yule hatatamani mke mwengine isipokuwa yeye ataenda mke yule kwa mganga mchafu na atataka usaidizi, akisahau kuwa Mwenyezi Mungu ndie ambaye amejaalia mapenzi ya dhati baina ya mume na mke hii ndio hali yetu waja wa Mwenyezi Mungu isipokuwa aliyerehemewa na Mwenyezi Mungu.

Ndugu katika imani ni vyema niwatajie Aya na hadithi za Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam). Amebainisha Mola katika Qur’an tukufu kwamba kujifundisha uchawi ni ukafiri.

قال تعالى) : وَمَا يُعَلِّمَانِ مِنْ أَحَدٍ حَتَّى يَقُولَا إِنَّمَا نَحْنُ فِتْنَةٌ) [البقرة: 102] Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Na hawamfundishi yoyote mpaka waseme hakika yetu sisi ni fitna usikufuru}}.

وقال تعالى) وَلَا يُفْلِحُ السَّاحِرُ حَيْثُ أَتَى) [طه: 69]

Vile vile Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Na hafaulu mchawi namna ajavyo}} [Twaha: 69]. Na amesema Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam): [ Jiupusheni na mambo saba yanayoangamiza, wakasema maswahaba: Ni yapi, ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu? Akasema Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam): Kumshirikisha Mwenyezi Mungu, uchawi, kula mali ya yatima, kukimbia vitani na kuwasingizia kuwa wamezini wanawake waliojihifadhi walioghafilika tena waumini].

Asema Aisha: [Watu walimuuliza Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) kuhusu uganga akasema: Hao si chochote. Wakasema: Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu hakika hao wanazungumzia mambo mara nyingine kisha yanatokea kweli. Akasema Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam): Hilo ni neno la haki analolichukua jinni kisha akalitia katika sikio la rafiki yake naye kwa upande wake akachanganya neno hilo na maneno mia ya uongo]. Na katika hadithi nyingine za kukataza uchawi na uganga. Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) amesema: [Atakayeenda kwa mganga au mchawi akamuuliza na akamuamini kwa atakayosema basi amekufuru aliyoteremshiwa Mtume Muhammad rehma na amani zimfikie].

Hadithi hii tukufu inatufundisha kwamba mtu yoyote atakaye kwenda kwa mganga kumuuliza kitu na akamuamini kwa atakayomwambia basi ametoka kabisa katika dini ya Uislamu. Ama hukumu ambayo inatakiwa aichukue kiongozi kwa atakayepatikana anafanya uchawi ni kukatwa shingo yake na kuuwawa kama ilivyothibiti katika maneno ya Maswahaba Mwenyezi Mungu awawie radhi; Tahadhari tunayoitoa ni kwamba haifai kwa Muislamu kuchukua hatua mikononi mwake isije ikaleta balaa na fujo miongoni mwa watu.

Madhara ya Wachawi na Waganga katika Umma

Ninafuraha enyi Waislamu, kutaja baadhi ya madhara ya waganga na wachawi katika umma. Madhara hayo ni kama yafuatayo;

Kufutika imani za wanaokwenda kwa waganga na kuwaamini kwa watakayo ambiwa kama ilivyo katika hadithi ya Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) tuliyoitaja.

Kukithiri vifo na au kuona makaburi yanafukuliwa au kuona baadhi ya viungo vya wanadamu kwa hawa waganga baada ya kuwaamrisha wafuasi wao wawaletee.

Kuenea zina na machafu baina ya watu kwani ni wangapi katika waganga hufanya zina na wake za watu na wakaharibu ndoa za watu na wakafungua milango mikubwa ya shari.

Kula mali za watu kwa njia ya batili kinyume na haki, kwani kila anachochukua mganga ni kwa kazi yake mbovu na anakula uchafu. Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam) amekataza kula thamani ya mbwa na mahari ya mzinifu na chumo la mganga.

Kuwapoteza watu na kuwafanya watu kuwa na tabia mbaya na kuwazuia wao kutekeleza maamrisho ya Dini, kwani kuna wengine huacha swala zote au baadhi yake na wengine huzuiliwa kuoga janaba na wengine huzuiliwa kufanya mema bali huamrishwa kufanya mabaya.

Kumkasirisha Mwenyezi Mungu na kusababisha adhabu yake. Alisema Zainab binti Jahshi kumwambia Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam): [Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Je tunaweza kuangamizwa na kati yetu kuna watu wema? Akasema Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam): Ndio, ukikithiri uchafu]. Na je kuna wachafu zaidi kuliko waganga waovu?.

Kupata hasara duniani na kesho akhera.

وقال تعالى) وَلَا يُفْلِحُ السَّاحِرُ حَيْثُ أَتَى) [طه: 69]

Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Na hafaulu mchawi namna ajavyo}} [Twaha: 69].

Sheikhul Islaam Ibn Taimia Mwenyezi Mungu Amrehemu amesema: «Hivi ndivyo ilivyo. Hakika ufuatiliaji unaonesha kwamba watu wakitegemea nyota hawafaulu. Si duniani bali vile vile kesho akhera.”

Hayo ndiyo baadhi ya madhara yanayopatikana kutoka kwa waganga waovu. Kwa hivyo, ni lazima ewe Muislamu kuelekea kwa Mwenyezi Mungu na watu wakumbushane kwamba jambo la kwenda kwa waganga na kuangaliliwa ni jambo baya na halifai. Jueni ya kwamba Mwenyezi Mungu ni Mfalme na Mwenye kumiliki kila kitu, hana wa kumzuwia anapo toa. Ametuamrisha Mola Wetu tutakapo kuwa na tatizo lolote tumuombe Yeye na tumtake Yeye msaada, na yafaa tumtegemee yeye katika kila kitu na tuchukue sababu za kisheria katika kufikia tunayoyakusudia na miongoni mwa sababu hizo ni kumuomba Mwenyezi Mungu dua. Kwa hivyo, atakaemuomba kwa nia njema hakika Mwenyezi Mungu hapotezi ujira wa amali ya anayeomba. Mwenyezi Mungu yuko karibu na hujibu maombi na yeye ndiye anayeruzuku ndege porini na samaki baharini.

قال تعالى) : اللَّهُ الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَأَنْزَلَ مِنَ السَّمَاءِ مَاءً فَأَخْرَجَ بِهِ مِنَ الثَّمَرَاتِ رِزْقًا لَكُمْ وَسَخَّرَ لَكُمُ الْفُلْكَ لِتَجْرِيَ فِي الْبَحْرِ بِأَمْرِهِ وَسَخَّرَ لَكُمُ الْأَنْهَارَ32 وَسَخَّرَ لَكُمُ الشَّمْسَ وَالْقَمَرَ دَائِبَيْنِ وَسَخَّرَ لَكُمُ اللَّيْلَ وَالنَّهَارَ) [إبراهيم32: 33]

Amesema Mola (Subhaanahu wa Taala): {{Mwenyezi Mungu ambaye ameumba mbingu na ardhi na ameteremsha maji kutoka mbinguni akatoa kutokana na maji hayo matunda hali ya kuwa ni riziki kwenu na Amewadhalilishia meli ili itembee baharini kwa amri Yake na Akawadhalilishia mito na akawadhalilishia jua na mwezi zinazotembea na akawadhalilishia usiku na mchana na akawapa kila mnachoomba na endapo mutazihesabu neema za Mwenyezi Mungu hamuwezi kuzidhibiti hakika mwanadamu ni dhalimu aliye mkufuru Mwenyezi Mungu}}.

Khutba ya pili

Kufuata Sababu Pamoja na Kumtegemea Mwenyezi Mungu

Shukrani za dhati ni za Mola Mlezi wa viumbe vyote. Rehma na amani zimfikie Mtume Muhammad. Ama baada ya kumshukuru Allah (Subhaanahu wa Taala) na kumtakia rehma na amani Mtume Wetu. Tumetaja katika KHUTBA YA KWANZA waliopewa mitihani ya matatizo, tukaweza kubainisha kwa kuzitaja Aya na hadithi zinazotoa tahadhari ya kwenda kwa waganga na wachawi pia tukaweza kutaja na kuweka wazi hatari na madhara ya waganga na wachawi katika jamii na mazingira tunayoishi tukaongezea kuwalingania watu kumuelekea Mwenyezi Mungu kwa kufuata sababu zinazoruhusiwa kisheria katika kukabiliana na matatizo mbali mbali.

Katika khutba hii ya pili napenda kurudia kwa kusisitiza sababu ambazo Ameziweka Allah (Subhaanahu wa Taala) kufuata ni dua, kumtegemea na kumtaka yeye pekee msaada. Kwani dua ni ibada na dua ni silaha ya Muislamu, Ametuamrisha Mwenyezi Mungu kumuomba yeye peke yake.

قال تعالى) : وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ فَلْيَسْتَجِيبُوا لِي وَلْيُؤْمِنُوا بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ ) [البقرة: 186]

Amesema Allah (Subhaanahu wa Taala): {{Na watakapoko uliza waja wangu kunihusu basi mimi niko karibu naitikia maombi ya anayeomba atakapoomba basi waniitikie mimi}}. Amesema mshairi kwamba Mwenyezi Mungu Anakasirika anapoombwa asiyekuwa yeye.

Ndugu Muislamu, Usiombe kabisa mwanadamu haja yoyote na muombe ambaye milango yake haifungwi. Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) Anakasirika ukiwacha kumuomba na ukimuomba mwanadamu anakasirika. Ewe unaye taka riziki, taka riziki kwa Mwenyezi Mungu.

قال تعالى) : فَابْتَغُوا عِنْدَ اللَّهِ الرِّزْقَ وَاعْبُدُوهُ وَاشْكُرُوا لَهُ إِلَيْهِ تُرْجَعُونَ) [العنكبوت: 17]

Amesema Mola (Subhaanahu wa Taala): {{Takeni riziki kwa Mwenyezi Mungu na muabuduni na mshukuruni kwake yeye mtaregea}}.

Ewe unaetaka kuzaa, Je umesahau dua ya Nabii Zakariya pale alipomuomba dua Mola wake akasema:

دعاء زكريا عليه السلام حين دعا ربه فقال) : (رَبِّ هَبْ لِي مِنْ لَدُنْكَ ذُرِّيَّةً طَيِّبَةً إِنَّكَ سَمِيعُ الدُّعَاءِ )[آل عمران: 38]

{{Mola wangu, Nipe mimi kutoka kwako kizazi kizuri hakika yako unaitikia maombi}}. Ewe unaye taka ufalme au cheo au chochote kile, kitake kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Tunapenda kuwakumbusha viongozi popote walipo na wenye ghera katika dini kwa majukumu waliyonayo kuhusiana na hawa waganga na wachawi na mafasiki katika kusimamishiwa hukumu ya Mwenyezi Mungu na kuwakataza watu kwenda kwa waganga na kuwakodishia maduka yao.

قال تعالى) : وَتَعَاوَنُوا عَلَى الْبِرِّ وَالتَّقْوَى وَلَا تَعَاوَنُوا عَلَى الْإِثْمِ وَالْعُدْوَ[([المائدة: 2] Kwani Mola (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Na saidianeni katika mema na uchaji Mungu wala musisaidiane katika madhambi na uadui}}. Amesema Sheikh Ibn Taimia Mwenyezi Mungu Amrehemu: “Na hakika imebainika katika tuliyoyataja kwa ujira unaochukuliwa kutoka kwa waganga, kuchukua hiba na karama ni haramu kwa anayetoa na anayechukua”. Kwa hivyo inatakiwa watu wakatazane jambo hili, kwani wakiwacha ibada hii ya kuamrishana mema na kukatazana maovu watapata hasara kubwa. Kwa kweli maovu yanaenea kiasi kikubwa ni kama ugonjwa ambao hautibiwi kwa kutumia dawa huzidi na kumdhoofika zaidi mwenye ugonjwa.

Tahadharisho kwa ndugu zangu Waislamu tusiliwache jambo hili tukawa kama Banii Israil ambao walikuwa hawakatazani maovu waliokuwa wakiyafanya ikawa ni sababu ya wao kulaaniwa.

قَوْلُهُ تَعَالَى : )كَانُوا لَا يَتَنَاهَوْنَ عَنْ مُنْكَرٍ فَعَلُوهُ) [المائدة: 79]

Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) Amesema: {{Walikuwa hawakatazani maovu waliokuwa wakiyafanya}}. Amesema Mtume (Swalla Llahu ‘alayhi wasallam): [Hakika watu watakapoona maovu na wasiliondoe inakaribia kujumuishwa na Allah kwenye adhabu yake].

Mwisho.

Nawausia ndugu zangu kumcha Mwenyezi Mungu na mtubie kwa Allah, mumtake msamaha na mtegemee yeye katika mambo yote pamoja na kufuata sababu za halali, wacheni kwenda kwa waganga na mujiepushe na jambo hilo hali ya kumtii Mungu na Mtume na kuhifadhi Dini yenu kwani leo ni kufanya vitendo bila kuhesabiwa na kesho ni hesabu bila kufanya vitendo.

Kwa ufupi katika khutba yetu hii tumezungumzia kufungamanisha nyoyo za Waislamu na Mola wao pia tumebainisha hukumu ya uchawi na uganga katika uislamu vile vile kutahadharisha watu kwenda kwa waganga na wapiga ramli, pia tumebainisha hatari za uganga katika umma na tumehimizana kufuata sababu za kisheria.

Mwisho tunamuomba Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala) atuhifadhi na kila balaa na Atuepushe na mitihani na matatizo. Atuongoze katika njia iliyonyooka, njia ya kukuelekeza katika dua na kufuata sababu za kisheria katika kutatua matatizo yetu..Ewe Mwenyezi Mungu itikia maombi yetu.





Vitambulisho: